SAMATTA AWATOA UDENDA ZAMALEK, WAWEKA DAU LA KUFURU
Klabu ya kongwe barani Afrika, Zamalek ya Misri imetoa kitita cha dola milioni 1 (zaidi ya Sh bilioni 2) kumsajili mshambuliaji Mtanzania, Mbwana Samatta anayekipiga TP Mazembe.
Samatta anayekipiga katika kikosi hicho cha matajiri wa DR Congo, anaweka rekodi ya kuwa mchezaji wa kwanza wa Tanzania, kupewa dili kubwa kama hilo la kununuliwa.
Tokea mchezo wa soka nchini uanzishwe, Samatta anayelamba dola 10,000 (zaidi ya Sh milioni 20) kwa mwezi, ndiye amefikia thamani ya mchezaji anayeweza kununuliwa kwa Sh zaidi ya bilioni moja.
Mwenyekiti wa Zamalek, Mourtada Mansour ameliamchia Championi Jumatatu katika mahojiano maalum kutoka Misri kwamba, wametoa kitita hicho cha dola milioni moja, ili wamnase Samatta na kuimarisha safu yao ya ushambuliaji.
Lakini akasema amekuwa na masikitiko makubwa baada ya kuambiwa Samatta amekataa kwenda kucheza Misri kwa kuwa asingependa kubaki Afrika tena.
“Kweli, tumetoa fedha hizo. Tunaamini hiyo ni thamani ya Samatta, tumempa heshima yake. Lakini bado inaonekana hataki tena kucheza Afrika baada ya kuondoka Mazembe. Huenda tutajaribu tena,” alisema Mansour.
“Bado tunaendelea kumshawishi, kama anataka kwenda Ulaya, hapa Zamalek ni lahisi kuonekana. Unawakumbuka akina Junior Agogo, Amri Zakh, Emanuel Amuneke, Mido na wengine wengi walitokea hapa.”
Taarifa hizo za kwamba Samatta amekataa fedha hizo, zilishitua gazeti hili ambalo lilifanya juhudi za kumpata kwa siku tatu lakini bila ya mafanikio.
Siku ya tano, Samatta alipatikana, safari hii akiwa nchini Morocco ambako TP Mazembe imeweka kambi kujiandaa na mechi za Ligi ya Mabingwa Afrika, pia ligi ya DR Congo.
“Ni kweli, Zamalek waliwasiliana na wakala na meneja wangu. Walitoa hiyo dola milioni moja, lakini bado nina mipango mingine,” alisema Samatta.
“Ningependa kutoka nje ya Afrika baada ya TP Mazembe. Hivyo ninaendelea kupambana kufikia ninachohitaji,” alisema Samatta akisisitiza anamuachia Mungu huku yeye akiendelea kujituma kwa juhudi kuu.
Samatta ni kati ya wachezaji waliocheza Ligi Kuu Bara kwa muda mchache sana lakini wana mafanikio makubwa sasa. Katika ligi hiyo aliichezea Simba akitokea Mbagala Market ambayo ilibadili jina na kuwa African Lyon baada ya kununuliwa na milione, Mohammed Dewji aliyekubali atue Simba wakati akiiuza.
SOURCE: CHAMPIONI
0 comments:
Post a Comment