YAJUE HAYA:VIDOKEZO MUHIMU BAJETI YA WIZARA YA ULINZI,, TANZANIA NI YA 20 AFRIKA KWA KUWA NA UIMARA WA JESHI,WAHINDI WAPIGWE MARUFUKU JESHINI
22:01 |
No Comments |
picha /maktaba |
WANAOMALIZA JKT WANAACHWA MTAANI BILA AJIRA,KUPIMA UKIMWI IWE LAZIMA JWTZ
WABUNGE wameendelea kuchangia hotuba ya Waziri
wa Ulinzi na Jeshi la Kutenga Taifa Dk. Hussein Mwinyi aliyoitoa jana.
Vifuatavyo ni baadhi ya vidokezo vilivyochangiwa na waheshimiwa wabunge
wa Bunge la 10 Jamhuri ya Muungano waTanzania, mkutano wake wa 15 kwenye kikao chake cha Saba.
Wataalamu tunao, tumewatelekeza- Anna Abdalah
MBUNGE wa Viti Maalum, Anna Abdalah amesema nchi imewatelekeza
wataalamu mbalimbali waliopo jeshini, ambao wanakaa kambini wakiwa
hawana kazi ya kufanya. Alisema baadhi ya zana za kivita zinaweza
kutengenezwa katika sehemu kama Nyumbu, lakini kutokana na ukosefu wa
fedha za kuendeshea kitengo hicho, matokeo yake askari hao wameendelea
kukaa kambini bila kazi na hivyo kutotumika kwa vipaji vyao.
Aidha,
mbunge huyo mkongwe alisema alama nyingi za mipakani ambazo ziliwekwa na
Jeshi zimeondolewa na hivyo kutojulikana wapi ni wapi, hasa katika
mipaka ya nchi jirani.
Wanaofariki nje hulipwa na nani?
Wabunge wamehoji juu ya askari wanaotumika kulinda amani katika
baadhi ya nchi duniani, kwamba wanalipwa na nani kati ya serikali au
Umoja wa Mataifa, kwani wanapokuwa huko, hutumika chini ya kofia ya UN.
Wametaka pia kujua idadi ya askari waliofariki dunia wakiwa katika utumishi huo nje ya nchi na kutaka kufahamishwa jinsifamilia zao zinavyolipwa fidia.
Mbona fedha za Jeshi zinacheleweshwa?
Wabunge pia wamezungumzia suala la Wizara ya Fedha kushindwa kupeleka
fedha za Wizara ya Ulinzi kwa wakati kwa visingizio kwamba fedha
hakuna, wakati inajulikana kuwa fedha zipo.
Walisema ni jambo la
hatari kwa nchi iwapo askari ambao hufanya kazi usiku na mchana kwa
ajili ya kulilinda taifa lao, litachoka kusubiri fedha, wakitolea mfano
kuwa mwaka jana walipokea kiasi cha asilimia 20 tu ya fedha zao za
bajeti.
Masilahi ya wastaafu yaliliwa
Kapteni Mstaafu wa Jeshi, John Chiligati amesema ulipwaji wa mafao ya
askari wastaafu wa Tanzania hauko vizuri na kupendekeza nchi ijifunze
kutoka India, kwani huko, licha ya kulipwa vizuri, lakini pia huwezeshwa kwa namna mbalimbali ili wasipate taabu katika maisha yao.
Alisema
kwa vile askari hustaafu kulingana na vyeo vyao, wale wenye ujuzi wa
aina mbalimbali, hutafutiwa kazi mbadala uraiani au kukopeshwa pesa na vyombo vya fedha ili waweze kujiajiri kwa kutumia taaluma zao uraiani.
Maonyesho ya Jeshi Dar yawagawa
Katika michango hiyo ya wabunge, baadhi yao walitofautiana kuhusiana
na maonyesho yaliyofanywa na Jeshi la Wananchi (JWTZ) wakati wa
maadhimisho ya miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, yaliyofanyika katika uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam April 26 mwaka huu.
Mmoja wa
wachangiaji hao alishangaa ni kwa namna gani Jeshi hilo liliweza kuanika
silaha zake hadharani, kwani kwa kufanya hivyo, ni rahisi kwa adui
kujua namna ya kukabiliana naye. Alikifananisha kitendo hicho na mtu
kuonyesha kila kitu chake hadharani, ikiwemo nguo yake ya ndani.
Hata
hivyo, wachangiaji wengine walisema maonyesho hayo ni jambo la kawaida
na kwamba baadhi ya nchi kubwa nazo hufanya namna hiyo, wakizitaja kama China, India na Marekani.
Wahindi wapigwe marufuku Jeshini
Mbunge mmoja alimtaka Waziri Mwinyi kuangalia uwezekano wa kuwaondoa
wafanyabiashara wa Kihindi katika maduka makubwa yaliyo ndani ya kambi
za kijeshi (Supermarkets) na kutaka kazi hiyo kupewa wazawa.
Huku
akisisitiza kuwa hakuwa mbaguzi wa rangi, alisema kazi za kuendesha
maduka hayo, tena ndani ya kambi za jeshi, inapaswa kufanywa na
watanzania wazawa, hasa kwa ajili ya kuimarisha ulinzi.
Aidha,
mbunge mwingine alishangaa na kuhoji kwa nini bei za bidhaa katika
maduka ya jeshi zimekuwa sawa na maduka ya uraiani wakati kule jeshini
kuna msamaha maalum wa kodi kiasi cha asilimia 18.
Hee, Tanzania ya 20 nguvu za kijeshi Afrika
Katika hali isiyotarajiwa, mbunge mmoja alisema licha ya mbwembwe
nyingi zilizoonyeshwa na Jeshi la Wananchi siku ya Muungano jijini Dar
es Salaam,
Tanzania ni ya 20 kwa majeshi yenye nguvu barani Afrika, kwa mujibu wa
mitandao inayozungumzia nguvu za majeshi duniani (hakutaja mtandao huo).
Alisema
katika mataifa yote duniani, Tanzania inashika nafasi ya 102 kwa nguvu
za kijeshi, huku akiponda kuwa nchi yetu inazidiwa hata na nchi za Uganda na
Rwanda ambazo zipo juu kimsimamo, kwa sababu ya kile alichosema
serikali kushindwa kuipa wizara husika fedha za kutosha kuweza
kujitosheleza.
Wanaopitia JKT, JKU janga la kitaifa
Baadhi ya wabunge pia walisema kuwaacha bila kuwapa ajira vijana
wanaomaliza mafunzo ya kijeshi katika majeshi ya JKT na JKU ni janga la
kitaifa kwa sababu wanapofika uraiani na kukutana na ugumu wa maisha,
wanaweza kufanya lolote ili kukabiliana na ugumu huo.
Walisema
wakiwa wanafahamu kutumia aina mbalimbali za silaha, ni rahisi kwao
kushawishika kwenda kushiriki matukio ya uhalifu, endapo atajitokeza mtu
na kuwaeleza juu ya uwezekano wa kupata kiasi kikubwa cha fedha.
Kwa ajili
hiyo, waliitaka wizara kuwapa kipaumbele vijana hao wanaomaliza mafunzo
katika ajira, ikiwa ni njia ya kusaidia kuokoa vijana ili wasijihusishe
na vitendo vya kihalifu.
Kupima Ukimwi iwe lazima JWTZ
Mbunge mwingine alisema kwa kuwa vijana wa JWTZ wana jukumu kubwa la
kuhakikisha mipaka ya nchi yetu inakuwa salama muda wote, wakati sasa
umefika kwa kila anayetaka kuajiriwa, lazima apimwe afya yake ili
kujiridhisha.
Alisema
jambo hili linapaswa kuzingatiwa hasa kwa vile kama hali itaachwa
iendelee hivi hivi, ipo siku taifa linaweza kujikuta likimpeleka mtu
mgonjwa vitani, ambaye anaweza kufariki kabla ya kufika katika uwanja wa
mapambano.
Aidha,
walisema wanajeshi wanapata ugonjwa huo kutokana na kuachwa nyuma kwa
wake au wapenzi wao wakati wanapohama kutoka kambi moja kwenda nyingine,
kitu kinachowafanya wachepuke.
Related Posts:
LHRC YAONYA KUHUSU PICHA ZA UCHI NA ZA KUTISHA Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimeonya vitendo vinavyofanywa na baadhi ya watu kuchapisha picha za utupu ama za kutisha katika … Read More
WAZIRI MKUU MAJALIWA AMWAKILISHA RAIS JOHN MAGUFULI KWENYE MKUTANO WA KUPAMBANA NA RUSHWA LONDON Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiongozwa kuingia kwenye ukumbi wa Lancaster House, London nchini Uingereza kuhudhuria mkutano wa Wakuu wa … Read More
TCRA : WATUMIAJI SIMU FEKI WAZIDI KUPUNGUA KUTOKA ASILIMIA 30 HADI 13 Kadri siku ya kuzima simu feki kote nchini inavyokaribia imebainika kuwa wanaozitumia wanazidi kupungua nchini. Meneja Mawasiliano wa Mamlaka … Read More
WAZIRI MKUU: SERIKALI ITAAGIZA TANI 70,000 ZA SUKARI Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Waandishi wa Habari kwenye makazi yake jijini Dar es salaam. (Picha na Ofisi ya Waziri M… Read More
TAMKO LA WIZARA KULAANI MAUAJI YA MAMA NA MTOTO, B/MOYO Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na watoto inasikitishwa na inalaani vikali tukio la kuuawa kwa kuchinjwa, mwanamke Oliver … Read More
0 comments:
Post a Comment