HATARI! WANAFUNZI VINARA WA KUNYWA GONGO NA VIROBA,KILIMANJARO
MKUU wa Wilaya ya Hai mkoani
Kilimanjaro, Novatus Makunga ameelezea hofu yake ya tishio la kukosekana
kwa nguvu kazi wilayani humo kutokana na kukithiri kwa wimbi la ulevi,
hasa wanafunzi wakiwemo wa shule za msingi wanaodaiwa kunywa kwa kiasi
kikubwa pombe aina ya gongo na nyingine za `viroba’
Kutokana na hali ya ulevi hata kwa watu
wazima, Makunga amesema miradi mingi ya maendeleo inakwama, hali
iliyomlazimu kupiga marufuku unywaji pombe saa za kazi, akitaka watu
wote waelekeze nguvu katika shughuli za ujenzi wa taifa.
Makunga aliyasema hayo jana wakati wa
maziko ya aliyekuwa Shekhe wa Mkoa wa Kilimanjaro, Ally Lema aliyefariki
juzi na kuzikwa jana nyumbani kwake katika Kijiji cha Uswaa, Kata ya
Uswaa wilayani Hai.
Aliwataka waombolezaji kufuata vyema
mafundisho ya viongozi wa dini ili kuepukana na mambo mengi yanayokwenda
kinyume na maadili, ikiwa ni pamoja na ulevi.
Mkuu huyo wa Wilaya alisema ameshangazwa
kuona idadi ndogo ya watoto katika shule mbalimbali, akitolea mfano
katika shule moja ya awali, kata nzima ilikuwa na watoto 15 tu.
“Nilipohoji sababu ya idadi ndogo ya
watoto hao katika shule ya awali, nilijibiwa kuwa inatokana na uzazi
hafifu, kwamba vijana wengi wamejikita katika ulevi kupindukia…hata kasi
ya kuzaliana kuwa ndogo. Lakini pia kwa shule nyingine, hali ya utoro
imekithiri,” alisema.
Kutokana na kukerwa na hali hiyo,
ameagiza kutungwa kwa sheria ndogondogo zitakazokataza matumizi hayo ya
pombe hizo wakati wa kazi na kuonya kuwa, mara baada ya sheria hizo
ndogo kupitishwa, kutakuwa na utaratibu wa kupekuliwa hadi kwenye mifuko
ya suruali na kwamba yeyote atakayekutwa na `viroba’ atachukuliwa
hatua.
Pia alisema mbali na sheria hizo, pia
ameagiza kurejeshwa kwa sheria za kuzuia baa na klabu za pombe
kufunguliwa na kuuza pombe nyakati za kazi.
Akizungumzia athari ya ulevi katika
kutekeleza miradi ya maendeleo, alisema akiwa wilayani Rombo katika
ziara ya kukagua miradi ya maji ya vijiji vitano hivi karibuni,
alijionea na kuelezwa jinsi mradi ulivyokwama kutekelezwa kutokana na
kukosa nguvu kazi, hasa vijana.