Tuesday 23 September 2014

HATARI! WANAFUNZI VINARA WA KUNYWA GONGO NA VIROBA,KILIMANJARO



MKUU wa Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro, Novatus Makunga ameelezea hofu yake ya tishio la kukosekana kwa nguvu kazi wilayani humo kutokana na kukithiri kwa wimbi la ulevi, hasa wanafunzi wakiwemo wa shule za msingi wanaodaiwa kunywa kwa kiasi kikubwa pombe aina ya gongo na nyingine za `viroba’

Kutokana na hali ya ulevi hata kwa watu wazima, Makunga amesema miradi mingi ya maendeleo inakwama, hali iliyomlazimu kupiga marufuku unywaji pombe saa za kazi, akitaka watu wote waelekeze nguvu katika shughuli za ujenzi wa taifa.

Makunga aliyasema hayo jana wakati wa maziko ya aliyekuwa Shekhe wa Mkoa wa Kilimanjaro, Ally Lema aliyefariki juzi na kuzikwa jana nyumbani kwake katika Kijiji cha Uswaa, Kata ya Uswaa wilayani Hai.

Aliwataka waombolezaji kufuata vyema mafundisho ya viongozi wa dini ili kuepukana na mambo mengi yanayokwenda kinyume na maadili, ikiwa ni pamoja na ulevi.

Mkuu huyo wa Wilaya alisema ameshangazwa kuona idadi ndogo ya watoto katika shule mbalimbali, akitolea mfano katika shule moja ya awali, kata nzima ilikuwa na watoto 15 tu.

“Nilipohoji sababu ya idadi ndogo ya watoto hao katika shule ya awali, nilijibiwa kuwa inatokana na uzazi hafifu, kwamba vijana wengi wamejikita katika ulevi kupindukia…hata kasi ya kuzaliana kuwa ndogo. Lakini pia kwa shule nyingine, hali ya utoro imekithiri,” alisema.

Kutokana na kukerwa na hali hiyo, ameagiza kutungwa kwa sheria ndogondogo zitakazokataza matumizi hayo ya pombe hizo wakati wa kazi na kuonya kuwa, mara baada ya sheria hizo ndogo kupitishwa, kutakuwa na utaratibu wa kupekuliwa hadi kwenye mifuko ya suruali na kwamba yeyote atakayekutwa na `viroba’ atachukuliwa hatua.

Pia alisema mbali na sheria hizo, pia ameagiza kurejeshwa kwa sheria za kuzuia baa na klabu za pombe kufunguliwa na kuuza pombe nyakati za kazi.

Akizungumzia athari ya ulevi katika kutekeleza miradi ya maendeleo, alisema akiwa wilayani Rombo katika ziara ya kukagua miradi ya maji ya vijiji vitano hivi karibuni, alijionea na kuelezwa jinsi mradi ulivyokwama kutekelezwa kutokana na kukosa nguvu kazi, hasa vijana.

OFFICIAL MEMBER

OFFICIAL MEMBER

Please Share This Site

HABARI ZETU

LIKE PAGE YETU HAPA