Tuesday 25 October 2016

TBL KUFANYA UZALISHAJI KWA KUTUMIA UMEME WA NISHATI YA JUA,YAANZA NA KIWANDA CHA MBEYA



Sehemu ya mitambo ya kisasa ya umeme wa jua iliyofungwa katika kiwanda cha TBL Mbeya,kiwanda bora cha kutengeneza bia barani Afrika.

 Katika mkakati wake wa kufanya uwekezaji wa mitambo inayotumia teknolojia ya kisasa na kufanya uzalishaji usiochafua mazingira,kampuni ya TBL Group imeanza kufanya uzalishaji wa bia kwa kutumia umeme unaotokana na nishati ya jua.

Uzalishaji wa kutumia umeme wa jua umeanza mapema wiki hii katika kiwanda cha bia cha Mbeya baada ya kukamilika kwa zoezi la kufunga vifaa vya kuvuna umeme wa jua kwenye kiwanda hicho vyenye uwezo wa kuzalisha umeme wa kilowati 138.

Mkurugenzi wa ufundi wa kampuni hiyo,Gavin Van Wijk, amesema kuwa teknolojia ya matumizi ya umeme unaotokana na nishati ya jua kuendesha kiwanda kikubwa kama hicho ni mpya hapa nchini na katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Alisema mitambo hiyo ya umeme wa jua imetengenezwa nchini Ujerumani na ina uwezo wa kuzalisha Kilowatt 138 na inao uwezo wa kukidhi mahitaji ya matumizi ya umeme wa kiwanda kwa asilimia zaidi ya 30%.

“Tumeanza kwa kufunga mitambo ya solar Panel 420 kwa awamu ya kwanza na tayari imeanza kuzalisha umeme wa kuendesha mashine za kiwanda na mwakani tutaongeza mitambo mingine ili umeme utakaozalishwa ufikie KiloWati 700 na ikifikia  hali hiyo kiwanda kitaendeshwa zaidi  kwa kutumia zaidi umeme wa jua kuliko wa sasa inaoupata kutoka Shirika la umeme Tanzania   ”.Alisema kwa kuwa mkoani Mbeya hali ya hewa ni nzuri na kuna vipindi vya jua kwa muda mrefu katika mwaka kuweza kupata nishati ya jua ya kutosha”.Alisema Gavin.

 Gavin alisema kuwa teknolojia hii haitaishia katika kiwanda cha Mbeya tu bali itatumika katika viwanda vingine vya kampuni hiyo “Tukimaliza Mbeya tutafunga mitambo hii katika kiwanda cha TBL cha jijini Mwanza kisha vitafuatia viwanda vingine.Tumejizatiti kuendelea kufanya uwekezaji wenye tija sambamba na mkakati wa serikali wa kuifanya Tanzania nchi ya viwanda.Kampuni inatumia zaidi ya dola milioni 14 kuwekeza katika mitambo inayotumia teknolojia ya kisasa”.Alisema.
Kwa upande wake Meneja wa kiwanda cha TBL cha Mbeya,Waziri Jemedari “Tunayo furaha kuona uwekezaji wa mitambo mikubwa ya kuvuna umeme wa jua katika ukanda wa Afrika Mashariki inaanza kufungwa katika kiwanda cha Mbeya.Tuna imani nishati ya umeme unaotokana na jua itapunguza kwa kiasi kikubwa gharama kubwa za uendeshaji ikiwemo kupunguza uchafuzi wa mazingira kwa njia ya hewa kutokana na uzalishaji”.Alisema Jemedari.

Aliongeza kuwa ufungaji wa mitambo hii ya kisasa yenye uwezo wa kuzalisha umeme mkubwa wa nishati ya jua wenye uwezo wa kuendesha mashine za viwanda unadhihirisha dhamira ya kampuni ya TBL ya kufanya uzalishaji usioathiri mazingira kama ambavyo kiwanda cha Mwanza tayari kimeanza kufanya uzalishaji wa kutumia nishati inayotokana na   pumba za mpunga.

0 comments:

Post a Comment

OFFICIAL MEMBER

OFFICIAL MEMBER

Please Share This Site

HABARI ZETU

LIKE PAGE YETU HAPA