SAMATTA NA ULIMWENGU WANUSURIKA KUFA DRC, WATU 15 WAFA PAPO HAPO BAADA YA VURUGU MECHI YA MAZEMBE NA AS VITA JANA
RAIS wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF), Issa Hayatou amesononeshwa na vifo vya mashabiki zaidi ya 15 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) baina ya wapinzani AS Vita Club na TP Mazembe mjini Kinshasa na amelitaka Shirikisho la Soka DRC (FECOFA) kuipa CAF ripoti kamili ya kilichotokea.
Katika
taarifa yake aliyoituma BIN ZUBEIRY leo, Hayatou amesema bodi hiyo ya
soka Afrika imesikitishwa na tukio hilo na kwamba wataweka mikakati ya
kudhibiti vurugu viwanjani wakati wa mechi.
![]() |
Poleni nyota wetu; Ulimwengu kulia na Samatta kushoto jana walinusurika kufa katika vurugu zilizochukua uhai wa watu 15 mjini Kinshasa, timu yao ikimenyana na AS Vita |
Hayatou ametoa pole kwa niaba ya CAF kwa
familia za waliofiwa kutokana na vurugu hizo, FECOFA na kusema anatumai
walioripotiwa kujeruhiwa wanapatiwa matibabu.
Juu ya hatua ambazo CAF itachukua kupambana
na vurugu viwanjani, Hayatou amesema: "Nataka kusema kwamba, aina
yoyote ya vurugu haina nafasi kwenye Uwanja wa soka. Lazima kuwe na
sheria kali na ninawaagiza Fecofa na mamlaka husika DRC kufanya
uchunguzi wa kina juu ya tatizo hili na kuhakikisha hatua kali
zinachukuliwa ili isijirudie aina yoyote ya tukio kama hili,”alisema
Mcameroon huyo.
Katika siku ya mwisho ya Ligi Kuu ya DRC
kwenye mchezo baina ya AS Vita Club na TP Mazembe Uwanja wa Tata Raphael
mjini Kinshasa jana, watu 15 walifariki dunia na wengine kibao
kujeruhiwa baada ya kutokea vurugu.
Vurugu hizo zilianza baada ya filimbi ya
mwisho ya mchezo huo, Mazembe yenye washambuliaji wawili Watanzania,
Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu ikishinda 1-0 na Polisi walijaribu
kutuliza vurugu hizo kwa kulipua mabomu ya machozi.
Gavana wa Kinshasa, Andre Kimbuta mara moja aliagiza uchunguzi ufanyike juu ya tukio hilo.
Vurugu hizo zinatokea wakati Mazembe na AS
Vita zimepangwa kundi moja katika Ligi ya Mabingwa Afrika na zitamenyana
tena Mei 25, mwaka huu mjini Lubumbashi katika michuano hiyo ya Afrika.
Mazembe iliifunga 4-1 Vita katika mchezo wa kwanza wa ligi ya DRC msimu
huu Lubumbashi na inahofiwa mashabiki wa timu ya akina Samatta watalipa
kisasi kwa mashabiki wa Vita Mei 25.
Chanzo: Bin Zubeiry
0 comments:
Post a Comment